Friday, 21 August 2015

Utafiti Wambeba Magufuli Urais 2015



Utafiti waonyesha Magufuli ana uwezo mkubwa wa kuwa Rais Na Mwandishi Wetu WAKATI kesho Chama Cha Mapinduzi(CCM) kikitarajia kufanya uzinduzi wa kampeni zake kwenye viwanja vya Jangwani, jijini Dar es Salaam, Taasisi ya Maendeleo, Vijana, Uongozi na Utawala Bora(YDG) imetoa utafiti na kuonyesha mgombea wa nafasi ya Urais wa CCM, Dk. John Pombe Magufuli anaongoza. Utafiti huo ulitolewa jana mjini Dar es Salaam na Katibu Mtendaji wa taasisi hiyo, Christopher Maganila, ambaye alisema katika utafiti walioufanya kuwa endapo uchaguzi mkuu ungefanyika leo, Dk Magufuli angeshinda nafasi hiyo. Alisema matokeo hayo, yanaonyesha Dk. Magufuli angeshinda kwa asilimia 45, huku mgombea wa CHADEMA Edward Lowassa angekuwa na asilimia 10.5, huku asilimia 35 wakisema hawajaamua mgombea gani anaweza kuwa Rais kwa kuwa ni bado mapema mno. Matokeo hayo pia yalionyesha kuwa wagombea wengine wangepata asilimia 0.1 hadi 5 huku asilimia 8 wakionekana wakisema hawajui ni mtu gani anafaa kuwa Rais kati ya wagombea waliochukua fomu za kuwania nafasi hiyo. “Huu ni utafiti huru na umefanikiwa kufika kwenye kila mkoa lakini kwa wilaya moja kwa kuwa tumeamua kuwahi ili kuona mwamko wa wananchi katika kupiga kura na kuchagua mgombea wanayemhitaji,’’alisema. Hata hivyo, Katibu huyo mtendaji alisema sababu nyingi walizoonekana kuzitoa wananchi kuwa Dk. Magufuli atakuwa mtendaji na mtu mwenye upeo mkubwa wa kufanya kazi endapo akipewa ridhaa. Kwa mujibu wa Katibu huyo, alisema anaamini uchaguzi wa mwaka huu, utakuwa huru na haki kwa kuwa wananchi wameonekana kuwa na mwamko katika kuchagua kiongozi atakayewaongoza.

Source: Jamii Forums